Njia Sita za Kupata Mafanikio
MTU anafanikiwa kikweli kwa
kupata njia bora kabisa ya maisha ambayo inatokana na kufuata viwango
vya Mungu na kuishi kupatana na kusudi la Mungu kwa wanadamu. Biblia
inasema kwamba mtu anayeishi maisha ya aina hiyo “atakuwa kama mti
uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika
majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zaburi 1:3.
Naam, ingawa sisi si wakamilifu
na tunafanya makosa, tunaweza kufanikiwa maishani! Je, hilo linakuvutia?
Ikiwa ndivyo, basi kanuni sita zinazofuata za Biblia zinaweza
kukusaidia ufikie lengo hilo na hivyo kuthibitisha waziwazi kwamba kwa
kweli mafundisho ya Biblia ni hekima inayotoka kwa Mungu.—Yakobo 3:17.
1 Uwe na Maoni Yanayofaa Kuhusu Pesa
“Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine . . . wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:10) Ona kwamba tatizo si pesa, kwa kuwa sisi sote tunahitaji pesa ili kujitunza na kutunza familia zetu. Tatizo ni kupenda pesa. Kwa kweli, upendo huo hufanya pesa ziwe bwana, au mungu.
Kama tulivyoona katika makala ya
kwanza ya mfululizo huu, watu ambao hukimbizana na utajiri ili wapate
mafanikio, kwa kweli wanafuatilia upepo. Mbali na kutamaushwa wanapatwa
na maumivu mengi. Kwa mfano, katika jitihada zao za kutafuta mali
nyingi, mara nyingi watu hupuuza uhusiano wao wa familia na marafiki.
Wengine hukosa usingizi, si kwa sababu ya kazi tu, bali pia kwa sababu
ya wasiwasi. “Usingizi wa kibarua ni mtamu, awe ameshiba au amekula
kidogo tu. Lakini usingizi wa tajiri ni wa wasiwasi daima, maana ziada
ya mali yake humsumbua usiku kucha,” inasema Mhubiri 5:12.—Biblia Habari Njema.
Zaidi ya kuwa bwana mkatili, pesa ni bwana mdanganyifu pia. Yesu Kristo alizungumza kuhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19)
Hilo linamaanisha kwamba utajiri humwahidi mtu kwamba utampa furaha,
lakini haufanyi hivyo. Badala yake unamfanya mtu atamani utajiri zaidi.
“Anayependa fedha hatatosheka na fedha,” inasema Mhubiri 5:10.
Kwa ufupi, mtu anayependa pesa anajiumiza tu. Anavunjika moyo, anakatishwa tamaa, au hata kujihusisha katika uhalifu. (Methali 28:20)
Ukarimu, kuwa tayari kusamehe, usafi wa maadili, upendo, na uhusiano
mzuri pamoja na Mungu, ni mambo yanayoleta furaha na mafanikio.
2 Sitawisha Roho ya Ukarimu
“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35)
Ingawa kuwapa watu vitu mara kwa mara kunaweza kumfanya mtu awe na
furaha ya muda, roho ya ukarimu inaweza kumfanya awe na furaha ya kudumu.
Ni kweli kwamba kuna njia mbalimbali za kuonyesha ukarimu. Mojawapo ya
njia bora na inayothaminiwa sana ni kutenga wakati ili kuwa pamoja na
watu na kufanya mambo nao.
Baada ya kupitia uchunguzi
mwingi kuhusu furaha, afya, na kutokuwa na ubinafsi, mchunguzi Stephen
G. Post alisema kwamba kutokuwa na ubinafsi na kuwasaidia wengine
kunahusianishwa na maisha marefu, afya nzuri kimwili na kiakili, kutia
ndani kupunguza kushuka moyo.
Isitoshe, watu wanaowapa watu vitu kwa ukawaida hawapungukiwi na chochote maishani kwa sababu tu ya kuwa wakarimu. Methali 11:25 inasema hivi: “Mtu mkarimu atafanikishwa, amnyweshaye mwingine maji naye atanyweshwa.” (BHN)
Kupatana na maneno hayo, watu ambao ni wakarimu kutoka moyoni, ambao
hawawapi watu vitu wakitarajia kulipwa, wanathaminiwa na kupendwa na
Mungu.—Waebrania 13:16.
3 Samehe kwa Hiari
“Endeleeni . . . kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.” (Wakolosai 3:13)
Siku hizi, watu hawako tayari kusamehe; wao hulipiza kisasi badala ya
kuonyesha rehema. Matokeo ni nini? Wanapotukanwa wanatukana, nao
hulipiza jeuri kwa jeuri.
Mambo hayaishii hapo tu. Ripoti moja katika gazeti The Gazette
la Montreal, Kanada inasema kwamba “katika uchunguzi uliofanyiwa watu
zaidi ya 4,600 wenye umri ya kati ya miaka 18 hadi 30,” wachunguzi
“waligundua kwamba uhasama, kukata tamaa, na kutokuwa na fadhili”
hufanya mapafu yawe mabovu. Kwa kweli, mambo hayo yanaweza kufanya
mapafu ya mtu kuwa mabovu zaidi kuliko ya mvutaji wa sigara! Bila shaka,
kusamehe hakufanyi iwe rahisi kushughulika na wengine tu bali pia
kunafaidi afya yetu!
Unawezaje kusamehe zaidi? Anza
kwa kujichunguza kwa unyoofu. Je, nyakati nyingine huwakasirishi watu?
Unafurahi wanapokusamehe? Kwa hiyo, mbona usiwaonyeshe wengine rehema? (Mathayo 18:21-35) Pia ni muhimu kujizuia. “Hesabu moja hadi kumi”
au tafuta wakati ili utulize hasira. Tambua kwamba kujizuia si udhaifu.
“Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu,”
inasema Methali 16:32. Maneno “ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu” yanaonyesha mtu amefanikiwa kikweli, sivyo?
4 Ishi Kulingana na Viwango vya Mungu
“Amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae.” (Zaburi 19:8)
Kwa ufupi, viwango vya Mungu vinatufaidi, kimwili, kiakili, na kihisia.
Vinatulinda dhidi ya mazoea yenye kudhuru kama vile, kutumia dawa za
kulevya, kulewa, ukosefu wa maadili, na kutazama ponografia (picha au
habari za ngono). (2 Wakorintho 7:1; Wakolosai 3:5) Huenda mazoea hayo yakatokeza madhara mabaya kama vile uhalifu, umaskini, kutoaminiana, kuvunjika kwa familia, matatizo ya kiakili na kihisia, magonjwa, na kifo cha mapema.
Kwa upande mwingine, wale
wanaoishi kulingana na viwango vya Mungu wanakuwa na mahusiano mazuri,
pia wanajiheshimu, na kuwa na amani ya akili. Katika Isaya 48:17, 18,
Mungu anasema kwamba yeye ndiye “anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe,
Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.”
Kisha anaongeza hivi: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako
ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” Ndiyo,
Muumba wetu anatutakia maisha bora zaidi. Anataka ‘tuende katika njia’
ya mafanikio ya kweli.
5 Onyesha Upendo Usio na Ubinafsi
“Upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1)
Je, unaweza kuwazia maisha yasiyo na upendo? Yangekuwa maisha yasiyo na
maana kama nini! “Ikiwa . . . sina upendo [kwa wengine], mimi si kitu.
. . . Sipati faida hata kidogo,” akaandika Paulo, mtume Mkristo
aliyeongozwa na roho ya Mungu.—1 Wakorintho 13:2, 3.
Upendo unaotajwa hapa si ule wa
kimahaba ambao una mahali pake panapofaa. Badala yake ni upendo unaodumu
ambao unaongozwa na kanuni za Mungu.* (Mathayo 22:37-39)
Isitoshe, mtu haonyeshwi tu upendo huo bali anauonyesha kwa matendo.
Paulo aliendelea kusema kwamba upendo huo ni wenye subira na pia
fadhili. Hauna wivu, haujigambi, au kujivuna. Hutafuta faida za wengine,
na hauchokozeki kwa urahisi bali ni wenye kusamehe. Upendo kama huo
hujenga. Pia, unatusaidia tuwe na uhusiano mzuri na wengine hasa
washiriki wa familia.—1 Wakorintho 13:4-8.
Kwa wazazi,
upendo unamaanisha kuwa na hisia nyororo kuwaelekea watoto wao na kuwapa
mwongozo ulio wazi unaotegemea Biblia kuhusu maadili na tabia nyingine.
Watoto wanaolelewa katika mazingira kama hayo hujihisi salama,
wanapendwa, na kuthaminiwa wakiwa sehemu ya familia iliyo imara.—Waefeso 5:33–6:4; Wakolosai 3:20.
Jack, anayeishi Marekani, ni
kijana aliyelelewa katika familia iliyofuata kanuni za Biblia. Baada ya
kuondoka nyumbani, Jack aliwaandikia wazazi wake barua. Sehemu ya barua
hiyo ilisema hivi: “Jambo moja ambalo nimejitahidi kufanya ni kufuata
agizo [la Biblia] linalosema: ‘Mheshimu baba yako na mama yako . . . ili
mambo yakuendee vema.’ (Kumbukumbu la Torati 5:16)
Mambo yameniendea vema. Na sasa ninathamini kwamba imekuwa hivyo kwa
sababu mlijitahidi kunilea kwa upendo. Asanteni sana kwa kunitegemeza na
kwa jitihada zenu nyingi za kunilea.” Kama wewe ni mzazi, ungehisije
kama ungepokea barua kama hiyo? Je, hungejawa na shangwe moyoni?
Pia, upendo unaotegemea kanuni ‘unashangilia pamoja na kweli,’ yaani, kweli kumhusu Mungu inayopatikana katika Biblia. (1 Wakorintho 13:6; Yohana 17:17) Ili kufafanua, fikiria mfano huu: Wenzi walio na matatizo katika ndoa yao wanaamua kusoma pamoja maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Marko 10:9:
“Kwa hiyo kile ambacho Mungu ameunganisha [katika ndoa] mtu yeyote
asikitenganishe.” Sasa, lazima wajichunguze mioyo yao. Je, kweli
‘wanashangilia pamoja na kweli za Biblia’? Je, wataiona na kuitendea
ndoa kama kitu kitakatifu, kama vile Mungu anavyoiona? Je, wako tayari
kujitahidi kutatua matatizo yao kwa upendo? Kwa kufanya hivyo wanaweza
kufanya ndoa yao ifanikiwe, na wanaweza kushangilia matokeo mazuri ya
jitihada zao.
6 Tambua Uhitaji Wako wa Kiroho
“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3)
Tofauti na wanyama, wanadamu wana uwezo wa kuthamini mambo ya kiroho.
Kwa sababu hiyo, sisi hujiuliza maswali kama haya, Ni nini kusudi la
uhai? Je, kuna Muumba? Ni nini hutupata tunapokufa? Wakati ujao
utakuwaje?
Ulimwenguni pote, mamilioni ya
watu wanyoofu wametambua kwamba Biblia inajibu maswali hayo. Kwa mfano,
swali la mwisho linahusiana na kusudi la Mungu kwa wanadamu. Kusudi hilo
ni nini? Ni kwamba dunia iwe paradiso inayokaliwa na watu wanaompenda
Mungu na viwango vyake. Zaburi 37:29 inasema: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”
Ni wazi kwamba Muumba wetu
anataka tufanikiwe kwa muda mrefu zaidi kuliko miaka 70 au 80 tu.
Anataka tufanikiwe milele! Kwa hiyo, sasa ndio wakati wako wa kujifunza
kuhusu Muumba wako. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee
kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule
uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3)
Unapoendelea kupata ujuzi huo na kuutumia maishani, utagundua kwamba
“baraka ya Yehova . . . ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja
nayo.”—Methali 10:22.
Comments
Post a Comment